LORI LAGONGA DALADALA, LAPARAMIA BAA NA KUUA WAWILI TEGETA...
https://roztoday.blogspot.com/2012/06/lori-lagonga-daladala-laparamia-baa-na.html
Lori lililokuwa limebeba kifusi limefeli breki na kugonga daladala kabla ya kuparamia baa iliyokuwa jirani na kusababisha vifo vya watu wawili papo hapo akiwamo mama lishe katika eneo la Tegeta Kibaoni, Dar es Salaam mchana huu.
Waliokufa katika ajali hiyo ni Mama Lishe, Halima Salumu mwenye miaka 35 na mwanaume mmoja ambaye hakutambulika jina aliyekuwa amesimama kituoni.
Ajali hiyo imetokea kwenye Njiapanda ya Kiwanda cha Wazo Hill ambapo lori hilo lenye namba za usajili T 376 AZH likiwa linatokea eneo la kiwanda hicho na kupamia daladala lenye namba T 761 AJC lililokuwa likipakia abiria kituoni hapo.
Baada ya kugonga daladala hilo lililokuwa likielekea Kariakoo, lililotumbukia mtaroni kisha kuvamia baa jirani ya KMM & Pub inayomilikiwa na Kuwedi Mongi na kumfunika mama ntilie huyo.
Akiwa kwenye eneo la tukio, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela mbali na marehemu hao, aliwataja majeruhi nane kuwa ni Peter Magayane, Frank Mmari, Ramadhani Rashid, Stanley Shenge, Agness Shadrak, Jane Kimaro, Anna Sahute na Ewina aliyefahamika kwa jina moja ambao wote walikuwa abiria katika daladala hilo linalofanya safari zake kati ya Kariakoo na Tegeta.
