"HAKUNA WANAJESHI WAVAMIZI KISIWA CHA UKEREWE"


Mandhari ya Kisiwa cha Ukerewe.

Baada ya Mbunge wa Ukerewe, Salvatory Machemli (Chadema), kuliambia Bunge kuwapo kwa askari wa Kenya na Uganda kinyemela kisiwani Ukerewe na kuhatarisha amani zipo taarifa kuwa hao ni maofisa uvuvi wa Afrika Mashariki. 
Imeelezwa kuwa maofisa hao wako kisiwani humo wakishirikiana na polisi wa nchini kukamata nyavu zilizopigwa marufuku kutumiwa ziwani kuvua samaki.
Machemli, ambaye jana aliomba Mwongozo wa Spika na kupewa nafasi, aliliambia Bunge kuwa askari hao wa nchi jirani, wamekuwa wakipiga wananchi na kuwadhalilisha kwa kisingizio cha kudhibiti uvuvi haramu.
Mbunge huyo alisema askari hao wamekuwa wakidai kutafuta nyavu ndogo, ambazo wanadai ni haramu kwa shughuli za uvuvi.
Kutokana na kauli hiyo, Spika Anne Makinda, aliagiza Serikali kutafuta uhakika wa habari za askari hao wa Kenya na Uganda kuingia kinyemela kisiwani Ukerewe na kutoa taarifa.
Kauli hiyo ya Spika ilikuja bungeni jana baada ya Machemli (Chadema), kutoa hoja bungeni akitaka Bunge lijadili kuhusu kitendo cha askari wa nchi hizo kuingia nchini kinyemela.
Spika Makinda alisema Bunge haliwezi kujadili hoja hiyo wakati Serikali haijafanya uchunguzi wa kutosha kuhusu kuingia kwa askari hao na kuagiza ifanye uchunguzi kuhusu suala hilo.
Hata hivyo, taarifa kutoka kwa Mwandishi Jovither Kaijage, aliye  Ukerewe, zilieleza kuwa hakuna uvamizi wa aina hiyo, isipokuwa ni operesheni dhidi ya uvuvi haramu, inayotekelezwa na maofisa uvuvi wa Tanzania, Kenya na Uganda.
Inadaiwa maofisa hao wakisaidiwa  na Polisi wa Kutuliza Ghasia (FFU),  wamevunja nyumba  na kupiga  wananchi kwa kisingizio cha kutafuta zana haramu za uvuvi.
Habari kutoka kata za  Ngoma, Bwiru  na Ilangala zilisema  kabla ya  uperesheni hiyo kufanyika  katika maeneo hayo, polisi walipiga risasi angani na kufyatua mabomu ya kutoa machozi.
Hali hiyo ilizua taharuki  na kusababisha watu wakimbie ovyo  huku wengine wakikamatwa  na kupigwa, wakati huo baadhi ya  milango ya nyumba zao ikivunjwa  na maofisa  hao kutafuta  zana haramu za uvuvi.
Mmoja wa  wafanyabiashara wa maduka katika  mwalo wa Bukimwi,  katika kata ya Ngoma, Ruigi  Ghatawa, alidai katika ghasia hizo juzi  mchana, duka  lake lilivunjwa na  fedha  Sh 270,000 kuibwa na watu hao. 
Ofisa Uvuvi wa Mkoa wa Mwanza, Lameck  Mongo, anayeongoza operesheni hiyo ya siku sita iliyoanza Januari 31, alikanusha tuhuma hizo za kuvunja nyumba na kupiga watu.
Hata hivyo, alikiri kuwa polisi walitumia mabomu kutawanya  wananchi ili wasidhuru maofisa hao wa doria na kuongeza kuwa wavuvi wanaonyang’anywa zana hizo haramu, ndio wanatoa taarifa hizo za uzushi ili waonekane wanaonewa.
Alisema wao hawakwenda Ukerewe kuonea watu, ila wanatafuta wahalifu na kuongeza kuwa ni lazima  zana hizo zitafutwe na kuharibiwa.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Ernest Mangu, mbali ya kuahidi kufuatilia ili kupata ukweli wa suala hilo, pia  alisema  hajapata taarifa hizo na kuongeza  kuwa  operesheni hiyo inatekelezwa  chini ya usimamizi wa  Mkuu wa Wilaya na ndiye anatakiwa kuulizwa suala hilo.
Mkuu wa Wilaya, Mary Tesha alipoulizwa , alipuuza madai hayo ya wananchi na kuongeza kuwa 
hivyo ni visingizio baada ya zana haramu walizokuwa wakimiliki kukamatwa na kuharibiwa.

Post a Comment

emo-but-icon

Follow Us

Hot Reads

Recent

Comments

Side Ads

Traffic

Text Widget

Connect Us

item