MTUHUMIWA SHAMBULIO LA BOMU KANISANI ARUSHA APEWA HATI YA MASHITAKA....
https://roztoday.blogspot.com/2013/06/mtuhumiwa-shambulio-la-bomu-kanisani.html
![]() |
| Victor Ambrose (kushoto) akiingia mahakamani chini ya ulinzi mkali wa polisi. |
Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Arumeru, Devotha Kamuzora jana alimkabidhi hati ya mashitaka yanayomkabili, Victor Ambrose (20) ambaye ni mtuhumiwa pekee aliyepandishwa kizimbani baada ya kutokea shambulio la bomu katika Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Olasiti jijini Arusha.
Ambrose alikabidhiwa hati hiyo ya mashitaka yanayomkabili jana katika Mahakama ya Wilaya ya Arumeru jijini Arusha na kuambiwa na wakili wa Serikali,
Adelaide Kasala kuwa upelelezi dhidi ya kesi hiyo, haujakamilika na kumuomba Hakimu Kamuzora kutaja tarehe nyingine tena.
Hakimu Kamuzora kabla ya kuahirisha kesi hiyo, alimuuliza Ambrose kama alipewa hati yake dhidi ya mshitaka yanayomkabili. Ndipo Ambrose alipojibu hapana. Baada ya jibu hilo ,Hakimu alitoa hati hiyo na kisha Ambrose kukabidhiwa na kuahirisha kesi hiyo hadi Juni 24 mwaka huu.
Ambrose ambaye ni dereva wa bodaboda na mkazi wa Mrombo jijini hapa, mara ya kwanza alifikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi jijini Arusha na baadaye kuhamishiwa Mahakama ya Wilaya ya Arumeru na kusomewa mashitaka yake kwa mara ya tatu sasa huku akitakiwa kutojibu lolote, kutokana na Mahakama hiyo kutokuwa na uwezo kisheria wa kusikiliza kesi za mauaji.
Wakili wa Serikali, Adelaide Kasala alidai mahakamani hapo Victor alitenda makosa hayo Mei 5, mwaka huu katika Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Olasiti jijini.
Alidai katika tukio hilo la mlipuko wa bomu, Victor aliwaua Regina Loning'o, James Gabriel Kessy na Patricia Joachim.
Pia, alidai alijaribu kuwaua Neema David, Harbart Njau, Regina David, Consesa Mbaga, Amarin Pius, Atanasia Reginald, Elizabeth Isdory, Alphonce Nyakundi, Joyce Yohana na Genesi Pius.
Wengine aliojaribu kuwaua ni Teofrida Innocent, Gabriel Godfrey, Manswet Siril Kessy, Editha Ndowo, Loveness Nelson, Dobora Joachim, Mathias Kiya na Restituta Alex Matemu.
